Sehemu kubwa ya mto huo iliyopo katika hifadhi ya taifa ya Ruaha
ambayo imesambaa katika mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya na Dodoma,
imekauka, huku maji yakionekana katika baadhi ya maeneo yametuwama na
kutengeneza madimbwi na katika baadhi ya maeneo yakitiririka kwa kasi
ndogo tofauti na hali yake ya kawaida yanapokuwapo ya kutosha.
Hali ya kukauka kwa mto huo iliwashtua wakuu wa mikoa ya Iringa,
Njombe na Mbeya, pamoja na wakuu wa wilaya za Kilolo, Ludewa,
Wanging’ombe, Makete na Njombe, waliofanya ziara ya kutembelea maeneo ya
mto huo mwishoni mwa wiki, na kujionea jinsi ulivyokauka na wanyama
wanavyoathirika kwa kukosa maji katika Hifadhi ya Ruaha.
Akizungumza na viongozi hao kabla ya kuanza kwa ziara hiyo
iliyoandaliwa na Shirika la Hifadhi la Kimataifa (WWF) kwa kushirikiana
na Bodi ya Maji ya Bonde la Mto Rufiji, Mratibu wa Maji wa WWF, Kevin
Robert, alisema lengo ni kuwawezesha viongozi hao ambao mto huo unapita
katika maeneo yao kuona kwa macho yao jinsi ulivyokauka ili waweze
kuchukua hatua za haraka kuunusuru kuanzia katika maeneo yao.
Alisema kukauka kwa mto huo kunatishia uhai wa wanyama na ekolojia
ya Hifadhi ya Ruaha na wananchi ambao wanategemea maji ya Mto Ruaha Mkuu
kuendesha shughuli zao za kiuchumi ikiwamo kilimo, kusababisha migogoro
ya kugombana rasilimali ndogo ya maji na kushusha uzalishaji wa umeme
katika mabwawa ya Mtera na Kidatu yanayotegemea kwa kiasi kikubwa maji
ya mto huo.
Naye Mhaidrolojia Bodi ya Maji Bonde la Rufiji, Grace Chitanda,
alisema kuanzia miaka ya 1994, Mto Ruaha Mkuu umekuwa ukikauka katika
eneo la kilomita 120 ndani ya wilaya ya Iringa pekee kila mwaka.
Alisema mto huo kwa kiasi kikubwa umeathiriwa na matumizi makubwa
ya maji kwa ajili ya shughuli za kilimo, kuingizwa mifugo kwa wingi hasa
katika maeneo chepechepe, matumizi ya viwanda, uchimbaji madini, makazi
katika vyanzo vya maji kiasi cha kuharibu mikondo ya mto na mabwawa,
upandaji wa miti aina ambazo hazihifadhi maji na uendeshai wa mitambo ya
umeme usiozingatia hifadhi ya mazingira kutoka katika mabwawa
yanayohifadhi maji hali inayohatarisha viumbe hai na hali ya mto.
Akitoa taarifa kuhusiana na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, Mhifadhi
Mkuu wa hifadhi hiyo, Dk. Chris Timbuka, alitaja baadhi ya athari za
kukauka kwa mto huo kuwa ni binadamu na wanyama kukosa maji, kupungua
kwa watalii, mivutano ya kugombea maji, kilimo kudumaa, uzalishaji umeme
kupungua, wanyama kuvamia makazi ya watu maeneo ya jirani kwa ajili ya
kutafuta maji na kuharibika kwa ekolojia ya hifadhi na wanyama kufa.
Wakizungumza baada kumaliza ziara ya kutembelea mto huo, viongozi
hao wakionekana kushtushwa na kile walichoshuhudia, walikubaliana
kuchukua hatua za haraka kunusuru hali hiyo, ikiwamo wakuu wa wilaya
kukabiliana na mambo yanayoathiri mtiririko wa maji na kusimamia sheria
za utunzaji mazingira katika maeneo yao.
Sign up here with your email
ConversionConversion EmoticonEmoticon