Kipande aliteuliwa Agosti mwaka 2012 na Dk. Harrison Mwakyembe
ambaye alikuwa Waziri wa Uchukuzi, baada ya kuwasimamisha kazi vigogo
sita wa TPA akiwamo Mkurugenzi Mkuu, Ephraem Mgawe, kutokana na tuhuma
mbalimbali za wizi.
Baada ya uamuzi huo, Sitta amemteua Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Awadhi Massawe kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPA.
Dk. Mwakyembe katika mabadiliko ya Baraza la Mawaziri yaliyofanywa
na Rais Kikwete Januari 25, mwaka huu, alihamishiwa Wizara ya
Ushirikiano wa Afrika Mashariki, wizara ambayo alikuwa akiiongoza Sitta.
Sitta akizungumza na waandishi wa habari jana katika ofisi za makao
makuu ya TPA jijini Dar es Salaam, alisema Kipande amesimamishwa kazi
kutokana na kukiuka taratibu za manunuzi na zabuni na kuwa na mahusiano
mabovu na wadau wa mamlaka hiyo.
“Tumekutana katika kikao cha dharura cha Bodi ya Bandari kutokana
na kuzingatia malalamiko ya sehemu mbalimbali kwamba taratibu za zabuni
TPA hazikukaa sawa, zinaendeshwa katika namna ambayo hazileti imani,
nampongeza Dk. Harrison Mwakyembe alianza vizuri kushughulikia suala
hili, lakini bado tatizo halijaisha,” alisema Sitta.
“Nimemsimamisha kazi kwa muda Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka
ya Bandari, Madeni Kipande leo hii (jana) Februari 16, 2015, ili
kupisha uchunguzi unaohusu tuhuma mbalimbali zinazomkabili,” alisema na
kuongeza:
“Tuhuma hizo ni pamoja na manung’uniko kuhusiana na ukiukwaji wa taratibu za manunuzi.”
Alisema TPA ni kituo muhimu cha uchumi wa nchi kwa sababu karibu
asilimia 87 ya mapato yanatoka hapo, hivyo kunahitajika watu kufanya
kazi kwa umakini na uadilifu zaidi.
Sitta alisema hapakuwapo na uwazi katika zabuni kiasi kwamba hata
baada ya Bodi ya Zabuni kufanya maamuzi kumekuwa na ucheleweshaji wa
kutoa barua ya kuidhinisha zabuni hizo, hivyo kuleta taswira mbaya kwa
serikali.
“Kwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Madeni Kipande ndiye msimamizi
mkuu wa masuala yote ya bandari kuanzia leo, namsimamisha kazi hadi hapo
tume niliyoiunda kuchunguza masuala hayo itakapokamilisha kazi,”
alisema.
Sitta alitangaza kamati aliyoiunda kuchukuza suala hilo kuwa ni
Jaji mstaafu Agusta Buheshi ambaye atakuwa Mwenyekiti na katibu wake ni
mfanyakazi wa Wizara ya Uchukuzi, Deogratius Kasinda.
Wajumbe wengine ni Dk. Ramadhani Mlingwa ambaye ni Mkurugenzi
mstaafu wa Mamlaka ya Manunuzi ya Umma (PPRA); Fravian Kinundo
(Mkurugenzi mstaafu wa Masoko TPA; Hapiness Senkoro na Mhandisi Samson
Luhigo ambao ni wafanyakazi wastaafu wa TPA.
Alisema ameamua kuwateua wastaafu katika kamati hiyo ambayo
itafanya kazi ya uchunguzi kwa muda wa wiki mbili kwa sababu watu hao
hawahitaji cheo.
Agosti 24, mwaka 2012, Dk. Mwakyembe aliifumua TPA kwa
kumsimamisha na baadaye kumfukuza kazi Mgawe na mabosi wengine sita
kufuatia tuhuma za ufisadi.
Wengine waliosimamishwa ni manaibu wakurugenzi wawili wa TPA ambao
ni Julius Mfuko (Maendeleo ya Miundombinu); Hamad Kashuma (Huduma);
Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Cassian Ng’amilo na mameneja wawili
wa Bohari ya Mafuta Kurasini Oil Jetty (KOJ) na mhandisi wa bohari
hiyo.
Dk. Mwakyembe alisema mabosi hao walisimamishwa kwa muda ili
kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali zinazoukabili uongozi wa bandari
ukiwamo wizi wa makontena, wizi mkubwa wa mafuta, udokozi wa mizigo na
rushwa katika utoaji wa huduma.
Alisema kumekuwa na wizi usioisha bandarini kiasi cha kutishia uhai
wake kwa kuwa unafukuza wateja ambao wamehamia bandari za Mombasa
nchini Kenya na Durban, Afrika Kusini ambako hakuna kero hizo.
Sign up here with your email
ConversionConversion EmoticonEmoticon