Katika tukio hilo, wanafunzi hao walimgomea Mkuu wa Wilaya ya Momba, Abiudi Saideya, alipowaomba watawanyike.
Wanafunzi hao kutoka Shule za Msingi Tunduma, Mlimani, Umoja na
Mwaka, waliandamana jana kuanzia saa 12:30 alfajiri na kuendelea kukaa
barabarani hadi saa 5:40 asubuhi wakiishinikiza serikali kuweka matuta
eneo la Mwaka lilikopo barabara kuu ya Tunduma – Sumbawanga jirani na
wanakosoma ili kuepusha ajali kuendelea kutokea.
Hatua ya wanafunzi kuandamana ilitokana na ajali ya lori lililokuwa
likitokea Sumbawanga kwenda Tunduma kuwagonga watatu na kusababisha
wawili kufa na mwingine kujeruhiwa vibaya.
Mmoja alikufa papo hapo na mwingine wakati akipatiwa matibabu Kituo cha Afya cha mjini Tunduma.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi, alisema mwanafunzi
Emmanuel Sichone, alifariki dunia papo hapo baada ya kugongwa na lori
hilo na Betiel Mbwambwa, alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu
kwenye kituo hicho.
Kamanda Msangi alisema mwanafunzi, Jackson Sichone amejeruhiwa vibaya na anaendelea kupatiwa matibabu kituoni hapo.
NIPASHE ambalo lililikuwa katika eneo hilo, lilishuhudia wanafunzi
hao wamekaa barabarani wakiimba nyimbo za kumtaka Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,
Abbas Kandoro, kufika kusikiliza madai yao.
Kabla ya Kandoro kufika, Mkuu wa Wilaya ya Momba, Saideya aliwasili kwenye eneo hilo.
Kabla ya kuzungumza nao, Diwani wa kata ya Tunduma, Frank
Mwakajoka, alisema eneo hilo ni hatari kwa maisha ya wanafunzi na
wananchi tangu barabara hiyo ilipojengwa.
Alisema hadi sasa wanafunzi 10 na watu wazima wanane, wamekufa kwa
kugongwa na magari, hivyo eneo hilo linahitaji kuwekwa matuta makubwa.
Alisema Januari 15, mwaka huu, alikwenda Ofisi za Wakala wa
Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Mbeya, kuomba yawekwe matuta eneo
hilo, lakini hadi sasa halijatekelezwa.
Mwakajoka aliliomba Jeshi la Polisi kuweka askari eneo hilo
kuwasaidia wanafunzi kuvuka barabara wakati Tanroads wakiendelea kujenga
matuta.
Akizungumza na wanafunzi hao, Mkuu wa Wilaya, Saideya, alisema
serikali imesikia kilio chao na itahakikisha matuta yanajengwa ili
kudhibiti magari kuendeshwa kwa mwendo wa kasi.
Alisema amewasiliana na Tanroads Mkoa wa Mbeya na wataalam wake
walikuwa njiani kutoka jijini Mbeya kuja Tunduma kuanza ujenzi wa matuta
hayo.
“Kuhusu askari kuwapo kwenye eneo hili, naagiza kuanzia sasa askari
wa Usalama Barabarani watakuwapo hapa kuanzia saa 2:00 asubuhi hadi saa
2:00 usiku kila siku kuhakikisha usalama unakuwapo. Niwahakikishie kuwa
matukio haya ya ajali sasa tutayadhibiti,” alisema Saideya.
Baada ya kutoa kauli hiyo, Saideya aliwaomba wanafunzi hao
watawanyike kurudi shuleni kuendelea na masomo, lakini waligoma huku
wakipiga kelele wakisema hawaondoki mpaka kieleweke.
Diwani Mwakajoka aliingilia kati na kuwasihi wanafunzi hao ambao
walichanganyika na vijana wa mtaani mjini Tunduma watawanyike na
kuwakumbusha msiba wa wenzao ambao miili yao ilikuwa bado haijazikwa.
Wanafunzi hao walikubali kuondoka barabarani ili kutoa nafasi kwa
serikali kutekeleza ahadi zake na kwenda kushiriki maziko ya wenzao
waliokufa kwa ajali.
Aidha, Mwakajoka alisema kuwa watoe nafasi kwa serikali kuweka
matuta hayo haraka na kwamba kama hayatawekwa kwa muda mwafaka, watarudi
tena barabarani kuandamana na kufunga njia.
Kauli hiyo iliwafanya wanafunzi na vijana wa mitaani kushangilia na
kuanza kuondoka barabarani na baada ya muda mfupi magari yaliyokuwa
yamezuiwa yalianza kupita kuendelea na safari zake.
Tafrani hiyo ilisababisha usumbufu mkubwa kwa wasafiri waliokuwa
wakitokea Sumbawanga kwenda Mbeya na wale waliokuwa wakitokea Mbeya na
mikoa mingine kwenda Zambia, Sumbawanga, Mpanda na Kigoma.
CHANZO:
NIPASHE
Sign up here with your email
ConversionConversion EmoticonEmoticon